Saturday, June 15, 2013

YAKO WAPI MAPENZI

Yako wapi mapenzi, uliyonipa tangiepo,
ukanitia uchizi, moy'angu ukauteka,
maisha yakawa matamu, honey likawa jina,
rudisha wako moyo, tuishi kama zamani.

vionjo ulivyonipa, adhimu kwa wengine
nkasahau katukatu, karaha za mapenzi
ukazidi nichanganya, kwa mungu nikaapa
Rudisha wako moyo, tuishi kama zamani

kwa mikogo n'katembea, mbele ya wenzangu
jeuri nikajijengea, ninaye mke mwema
hakika sikuiota, siku n'takayotendwa
Rudisha wako moyo, tuishi kama zamani

wenzangu zikawapaa, mioyo mpwitompwito
likawatia wazimu, wakazidi chachalika
chokochoko wakatia, penzile' kuharibu
Rudisha wako moyo, tuishi kama zamani

kwangu ukajiapiza, hutong'atuka katu!
nanga kwangu umetia, mithili manowali
wazimu nikajitia, manenoyo n'kasadiki
Rudisha wako moyo, tuishi kama zamani

hakika sikujua, maneno ya wahenga,
kila king'aacho, 'sidhani ni dhahabu
kivumacho hakidumu, msumari wakapigia
Rudisha wako moyo, tuishi kama zamani

maneno ya wapambe, yakaanza kukulevya
ukaanza kukacha, penzi njiani kutelekeza
ukaniacha ka' hayawani, kinda la dege tawini
Rudisha wako moyo, tuishi kama zamani

roho i radhi, bali mwili dhaifu
penzilo siwezi hacha, pekee n'kaishi
utanitia wazimu, kitanzi nijitie
Rudisha moyo Pepe, tuishi ka'zamani

Nani alokuloga, Pepe ukasaliti
moyoni nitoa, ukasahau zamani
ukajitia ukiziwi, kutosikia hiki kilio
Haya hii pen, nakuandikia mpenzi

Hakika nimekua, ya wakubwa 'meng'amua
mla mla leo, mla jana kala nini?
japo jana nilikula, mwenzio leo ni' taabuni
Rudisha wako moyo tuishi kama zamani

Mwandishi/mtunzi: John Jonas R.

No comments:

Post a Comment